Breaking News

WANANCHI WAGOMA KUMPA FEDHA MBUNGE ILI AWAPELEKEE KATIBA YA SASA.

Katibu Mtendaji wa Rango, Stanley Mshana, akitoa mada katika Mdahalo wa kuhamasisha wananchi kujitokeza kushirika katika mchakato wa kupata katiba mpya jana katika kijiji cha Majalila wilayani Mpanda
WANANCHI wanaoishi vijiji vya tarafa ya Kabungu, jimbo la Mpanda vijijini,
mkoa mpya wa Katavi wamekataa hoja ya kuchanga fedha kiasi cha Sh 7000 na
kumkabidhi mbunge wao, ili aweze kuwanunulia nakala ya Katiba ya sasa kwa
madai kuwa kufanya hivyo kutawafanya wawe watumwa dhidi ya mwanasiasa huyo.

Kauli hiyo ya wananchi hao ilikuja baada ya mjumbe wa bodi ya Muungano wa
taasisi zisizo za kiserikali (Rango) na mratibu wa masuala ya elimu wa haki
za binadamu wilaya ya Mpanda, Suleiman Tumaini kutoa ushauri huo kwa
wananchi hao. wakati akitoa mada katika mdahalo wa kuhamasisha wananchi
wajitokeze kutoa maoni ya juu ya mchakato wa kupata katiba mpya,
ulioandaliwa na Taasisi hiyo chini ya ufadhili na shirika la The Foundation
for Civil Society na kufanyika katika shule ya Msingi Mpanda ndogo.

Mmoja wa wananchi hao, Milambo Iddy alisema kuwa si sahihi wananchi
kuchanga fedha na kumkabidhi mbunge huyo ili aweze kutuletea nakala ya
katika kwa kuwa hazitafika kwa wakati kutokana na kuwa na kutumia muda
mwingi katika vikao vya bunge, shughuli zake binafsi na chama cha ushirika
ukizingatia kwamba yeye ni Mwenyekiti wa vyama vya ushirika vya wakulima wa
tumbaku.

"Nimesikia mtoa mada anasema kama tunataka nakala za katiba ya sasa,
tuchange fedha na kumkabidhi mbunge wetu atununulie na kutuletea...... sasa
msimamo wetu ni kwamba hatuko tayari kufanya hivyo kwa kuwa tutakuwa
watumwa kwake wa nenda rudi maana ana shughuli nyingi, matokeo yake hizo
nakala za katiba hazitatufikia wakati mwafaka...... badala yake tunataka
maduka yafunguliwe katika kata na vijiji na kuuza hizo nakala za katiba
kama ambavyo bidhaa nyingine zivyonauzwa" Alisema.

Iddy aliongeza kuwa wana mahitaji makubwa ya kupata nakala za katiba ya
sasa kwani vinginevyo hawataweza kutoa maoni kwa usahihi zaidi wakati tume
itakapopita kukusanya maoni ya uundwaji wa katiba mpya kwa kuwa ya sasa
ambayo imepigiwa kelele kwamba imepitwa na wakati hawajawahi kuisoma na
hawajui mapungufu yake.

Kauli hiyo iliungwa mkono na Sudi Kasapa ambaye alisema kuwa pamoja na
mahitaji makubwa waliyonayo ya kupata katiba hiyo, lakini kamwe hawezi
kuchanga fedha na kumpatia mbunge huyo kwa kuwa hawezi kuzifikisha kwa
wakati hivyo wanaweza kukosa fursa ya kusoma kwa makini na kubaini
mapungufu yaliyopo lakini zikiuzwa madukani wako tayari kununua.

Aidha Kasapa alisema kuwa suala la katiba wasiachiwe wanasiasa pekee
kulipigia kelele lakini badala yake ipo haja kwa wananchi hasa vijijini
kuelimishwa zaidi umuhimu na faida ya kupata katiba mpya kwa kuwa wengi wao
hawajui kitu chochote kuhusu katiba hiyo.

Hata hivyo baada ya kugoma kupitishia fedha watakazochanga kwa mbunge
huyo,Mjumbe huyo wa Rango aliwataka wananchi hao kumpatia yeye mwenyewe na
kisha ataagizanakala za katiba hizo mjini Sumbawanga kisha kuwafikishia
kupitia kwa afisa tarafa, hoja ambayo wananchi hao walikubaliana nayo.

Naye, Katibu Mtendaji wa Taasisi hiyo , Stanley Mshana, aliwahimiza
wananchi hao kujitokeza kwa wingi mara baada ya tume ya kukusanya maoni juu
ya katiba mpya itakapoanza kufanya kazi ili waweze kushiriki ipasavyo
katika mchakato huo na si kalalamika pasipo kuonyesha ushiriki wao.

Alisema kujitoa na kutoshiriki katika utoaji wa maoni ni kujisaliti wenyewe
kwakuwa kunaweza kusababisha kuundwa kwa katiba isiyoweza kutatua kwa
asilimia kubwa changamoto zilizopo kwenye maeneo yao.

No comments