Breaking News

WATU WASIOJULIKANA WAVAMIA LUSAKA SEKONDARI NA KUFANYA UHARIBIFU MKUBWA.

WATU   wasiojulikana  wanadaiwa  kuvamia katika  Shule  ya Sekondari  ya  Lusaka iliyopo kata ya Lusaka  wilayani  Sumbawanga  na  kufanya  uharibifu  mkubwa  wa  majengo  na  kuiba vitu mbalimbali vilivokuwa kwenye  stoo  ya   shule  hiyo.

Kwa mujibu  wa Kaimu  Mkurugenzi  wa halmashauri  ya  Wilaya  ya Sumbawanga Crispin  Luanda  uvamizi  na  uhalibifu huo  ulifanyika Usiku wa kuamkia Desemba 27 mwaka jana.


Kufuatia  taarifa  za   uhalifu  huo timu ya wataalamu kutoka ofisi ya mkurugenzi ikiongozwa na Kaimu Mkurugenzi  wa Halmashauri  hiyo , Luanda ilitembelea shule hiyo na kushuhudia uharibifu mkubwa uliofanywa na wavamizi hao, ambapo suala hilo linafanyiwa kazi na halmashauri kwa kushirikiana na vyombo vya usalama.


Kwa mujibu  wa Luanda , tathimini ya awali  iliyofanyika  imebaini kuwa hasara iliyopatikana  kutokana  na  uhalibifu  wa majengo  wa  shule  hiyo ni Sh  2,570,000.


“Uharibifu uliofanywa ni kuvunjwa kwa vioo vya madirisha katika ofisi ya Mkuu wa shule pamoja na kuvunjwa kwa vioo vya madirisha katika nyumba  mbili za walimu ikiwemo ya mkuu wa shule.


Wahalifu hao pia walivunja stoo ya shule na kuiba mahindi kiasi cha gunia moja na debe tatu yaliyokuwa yakitumiwa na wanafunzi wa shule hiyo’ alisema Luanda


Kaimu  Mkurugenzi  huo  alitanabaisha  kuwa wakati wa tukio hilo linalodhaniwa kufanywa  saa nane  za usiku,walimu walikuwa ndani wamelala na baada ya kugundua kuwa wamevamiwa walianza kuwasiliana kwa simu za mkononi na kupeana taarifa kabla ya wavamizi hao kutokomea kusikojulikana.


Kwa  mujibu  wa  Kamanda  wa Polisi  wa Mkoa  wa Rukwa , Isuto Mantage  hadi  sasa  hakuna  aliyekamatwa   kuhusiana  na  tukio  hilo  kwamba   uchunguzi  na  msako  wa  kuwabaini  wahalifu  hao  unaendelea  ili  sheria   iweze kuchukua   mkondo  wake.


Shule  hiyo  ya Lusaka  imekuwa  ikikumbwa  na  mikasa  ya  mara  kwa mara ambapo   Machi 19  mwaka  jana  Serikali  iliamua   kuifunga  shule  hiyo  kwa  muda usiojulikana baada ya wanafunzi kutaka kuwaua walimu wao kwa kuwachoma na moto wakiwa wamelala.

Kaimu Mkururgenzi wa wilaya ya Sumbawanga, Crispin Luanda (wa pili kulia) akikagua uharibifu uliofanywa katika shule ya sekondari Lusaka iliyopo wilayani Sumbawanga baada ya watu wasiojulikana kuvamia shule hiyo hivi karibuni.Kulia ni ofisa utumishi, John Maholani, kushoto ni mkuu wa shule hiyo, Jonasio Simsokwe na Afisa Elimu, Emanuel Kipele

No comments