Breaking News

Rukwa wataka kura ya hapana kwa Katiba Pendekezwa

Mchungaji wa KKT ushirika wa Sumbawanga mjini mkoani Rukwa, Calvin Kessy akichangia mada kuhusu katiba pendekezwa.
BAADHI ya Wananchi mkoani Rukwa, wamesema kuwa Katiba Pendekezwa imeepuuza maoni ya wananchi badala imeandaliwa kwa ajili ya kulinda maslahi ya watu wachache hivyo haipaswi kupigiwa kura ya ndio.

Wamesema hayo kwa nyakati tofauti jana wakati wakichangia mada katika mafunzo ya elimu ya uraia kwa mpiga kura kuhusu katiba inayopendekezwa, yaliyoandaliwa na Taasisi isiyo ya kiserikali ya Kituo cha sheria na Haki za Binadamu, yakiwalenga viongozi wa dini ambayo yaliyofanyika kwenye ukumbi wa kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKT) lililopo mjini hapa


Washiriki wakifuatilia mada mbalimbali kuhusu Katiba Pendekezwa.
Mmoja wa waliotoa maoni yao ni Mchungaji wa KKT ushirika wa Sumbawanga mjini mkoani Rukwa, Calvin Kessy, alisema kuwa Katiba Pendekezwa imepuuza maoni ya watanzania walio wengi kiasi kwamba ni dhambi kubwa kwa mungu kumshawishi mtu aende kuipigia kura ya ndio.

Alisema mathalani kupuuzwa kwa maoni ya watanzania kumeanzia kwenye muundo wa Serikali ambapo maoni ya walio wengi walitaka muundo wa serikali tatu ambao ndio ungetambua uwepo wa serikali zote tatu yaani ya Zanzibar, Tanganyika na Muungano.

Alisema kuwa cha kushangaza hivi sasa Katiba hiyo imerudisha Serikali mbili yaani Zanzibar na Muungano pasipo Serikali ya Tanganyika ambayo watanzania wengi wamekuwa wakililia hivyo ukipiga kura ya kupitisha Katiba hiyo, maana yake unaunga mkono maslahi ya wachache wasioitaka serikali ya Tanganyika kwa manufaa yao tu.

Mwanasheria kutoka kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, Fered Lyimo akiwasilisha mada.
Mchungaji Kessy alitaja jambo jingine lililopuuzwa na halipo katika katiba pendekezwa ni kumwajibisha Mbunge ambapo katika maoni yao walitaka mbunge awajibishwe kwa kupigiwa kura ya kutokuwa na imani nae kama akienda kinyume na maslahi ya wananchi wa jimbo husika.

"Lipo tatizo la mbunge anaomba ridhaa ya kuchaguliwa katika jimbo fulani akipata ubunge anaondoka kwa miaka kadhaa....... sasa kwa kuona hivyo wananchi walipendekeza apigiwe kura ya kutokuwa na imani nae kwa kuwa kama yeye ni mtumishi na tayari amekuwa hayupo katika kituo chake cha kazi basi hawajibishwe kama watumishi wengine wa umma wanavyowajibishwa lakini si kusubiri miaka mitano" alisema.

Washiriki wakifuatilia mada mbalimbali kuhusu Katiba Pendekezwa.
Naye, Mchungaji Charles Ahombile akizungumza kwa masikitiko makubwa alisema kuwa bunge la katiba limeacha mambo mengi ya msingi moja wapo likiwa ni  sifa ya kielimu ya mbunge ambapo maoni yao yalitaka mbunge awe na elimu kuanzia kidato cha nne kwenda juu na ajue kusoma na kuandika lugha Kiswahili na Kingereza lakini Katiba Pendekezwa imendekeza sifa ya mbunge kujua kusoma na kuandika lugha ya kiswahili na Kingereza.

Alisema utashangaa kabisa unakuta dereva wa mbunge ana elimu ya kidato cha nne ila mbunge ni darasa la pili au la saba kitu ambacho ni aibu na katiba pendekezwa haijayatendea haki mapendekezo ya wananchi badala yake wabunge wamejitazama wao tu kwa maono ya leo lakini si ya miaka 50 ijayo ya katiba hiyo.

Mchungaji Charles Ahombile akichangia mada
Awali, akitoa mada Mwanasheria kutoka kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, Fered Lyimo alisema kuwa wananchi wanapaswa kuisoma na kuielewa Katiba Pendekezwa kabla ya kufanya maamuzi ya kupiga kura pamoja na kwamba vipo baadhi ya vyama vya siasa vinashawishi wananchi kupiga kura ya ndio.

Aliongeza kuwa chama kinachotaka wananchi wapige kura ya ndio kabla ya kuisoma katiba kinajua udhaifu mkubwa uliopo hivyo hawataki wananchi wajue ndio maana wanashinikiza ukifika wakati ipigwe kura ya ndio kitu ambacho hakipaswi kushabikiwa na wananchi kwa kufanya hivyo  kabla ya kuisoma na kuielewa ni hatari sana ustawi wa taifa hili.

No comments